Featured Post

HALMASHAURI KALIUA YATOA MIKOPO SHILINGI MILIONI 240

MATANGAZO

Wednesday, December 1, 2021

HALMASHAURI KALIUA YATOA MIKOPO SHILINGI MILIONI 240


 Robert Kakwesi,Tabora

Tabora.   Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua,watu wake wamehamasika kwa kuunda vikundi vya  wajasiriamali 826 vyenye wanachama 8,820 ambavyo vinahitaji mikopo kutoka asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa ajili ya makundi maalum ya wanawake,vijana na watu wenye ulemavu.

Kutokana na hamasa kubwa iliyopekea idadi kubwa ya vikundi,mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo,Jerry Mwaga,anasema halmashauri inakabiliwa na changamoto kubwa kwani uwezo wake ni kutoa mikopo kwa vikundi 45 kwa mwaka.

Akizungumza wakati wa Utoaji Hundi yenye thamani ya Sh240milioni kwa vikundi vya wanawake,vijana na watu wenye ulemavu 32,amesema sekta ya maendeleo ya Jamii ikutumika vizuri ,inaweza kuleta maendeleo Chanya na haraka kwa jamii.

"Fursa hii muhimu na adhimu ni lazima itumike vizuri kwa manufaa ya wahusika na jamii mzima kwa ujumla"Amesema

Mkurugenzi Mwaga pia amesema wanatoa hata vifaa kwa ajili ya wajasiriamali ambao 15 wamekabidhiwa pikipiki kwa ajili ya Biashara ya bodaboda huku watendaji 25 wakikabidhiwa pikipiki 25 kwa ajili ya utendaji kazi na kufanya zote 40 kuwa na thamani ya Sh69milioni.

Akikabidhi Hundi na pikipiki,mkuu wa mkoa wa Tabora,Dk Batilda Burian,amewahimiza wajasiriamali kurejesha mikopo kwa wakati ili na wengine na vikundi na wenyewe waweze kukopa.

Amewaasa kutofanya kiburi kwa kusubiri Hadi waanze kufuatwa au kutaka kupelekwa mahakamani ndio waanze kurejesha.

"Fursa hii mnayopata muitumie vizuri huku mkikumbuka na wengine wanasubiri mrejeshe ili nao wakope kamwe msisubiri mfuatwe au kutaka kupelekwa mahakamani ndio mrejeshe"Amesema.

Katika vikundi hivyo,vikundi  11 vya wanawake na vikundi 8 vya vijana ,vyote vikipata jumla ya Sh192milioni wakati vikundi 13 vya watu wenye ulemavu vikipata jumla ya Sh48milioni.


Tuesday, November 23, 2021

WILAYA YA KALIUA YAWAPUNGUZIA WAJAWAZITO KUJIFUNGULIA WILAYA JIRANI

 



Robert Kakwesi, Tabora

Hospitali ya Wilaya ya Kaliua,imehudumia wajawazito zaidi ya 300 katika kipindi Cha miezi kumi tangu kuanza kwake kutoa huduma.

 Katika kipindi hicho watoto zaidi ya mia tatu wamezaliwa huku wengine wakizaliwa kwa njia ya upasuaji.

 Tangu kuanzishwa kwake kuwa Wilaya mwaka 2014 ,Kaliua haikuwa na hospitali ya Wilaya baada ya kugawanywa iliyokuwa Wilaya ya Urambo na kuunda Wilaya mbili za Kaliua na Urambo.

 Kutokana na kutokuwa na hospitali yake ya Wilaya,wananchi wanaougua walikuwa wanalazimika kwenda Wilaya jirani za Uvinza,Urambo na Tabora umbali wa Hadi kufikia zaidi ya km120 na hivyo wagonjwa na wananchi kuteseka na kutumia kiasi kikubwa Cha fedha.

 Hata wajawazito nao wakilazimika kusafiri umbali mrefu kufuata huduma ya kujifungua na pale wanapolazimika kufanyiwa upasuaji Hali kuwa ngumu zaidi.

 Mganga mkuu wa halmashauri ya Wilaya ya Kaliua,Dk Lusubilo Adam,amesema wamehudumia kati ya wajawazito 300 Hadi 350 tangu waanze kutoa huduma.mwezi wa kumi mwaka Jana na kufanya zaidi ya wateja 700 kuhudumiwa wakiwemo wale wasiolazwa.

 "Mbali na kutoa huduma kwa wagonjwa na wajawazito,tumefanya upasuaji kwa wagonjwa wapatao hamsini na tunatoa huduma zilizo Bora"Amesema

 Dk Lusubilo ameongeza kuwa Wana wodi kubwa ya wajawazito inayoweza kuhudumiwa wajawazito 48 kwa wakati mmoja na kwamba dawa zipo na wataalamu wapo.

 Ameeleza kuwa wataanza kutoa huduma ya kulaza wanaume na watoto na pia huduma ya kuhifadhi maiti kwani majengo yake yamefikia hatua za mwisho kukamilika.

 Amesema kuanza kutoa huduma ya kulaza na kuhifadhi miili,kutawapunguzia gharama na muda wananchi waliokuwa wakifuata huduma wilaya jirani za Urambo na Tabora.

 Mmoja wa wanawake waliojifungua Hospitalini hapo,Zaituni Shaban,mkazi wa Ushokola,Amesema kwa kupata huduma hapo,wanaokoa fedha ambazo zinafanya shughuli zingine.

 "Tulikuwa tunapata shida ya kwenda Urambo na huko ndugu inabidi walale na kulazimika kutumia fedha nyingi tofauti na hapa"Amesema

 Mkazi wa Kazaroho,Mwanaidi Hassan,amesema mtoto wa jirani yake,alifariki baada ya kukosa huduma ya upasuaji kutokana na kukosa usafiri wa gari la kumkimbiza Wilaya Jirani ya Urambo.

 "Kama angepata usafiri Tena mapema,wangeweza kuokoa maisha yake ingawa kwa Sasa tunafurahi huduma ya upasuaji kufanyika hapa Kaliua"Amesema.

 Mwenyekiti wa halmashauri ya Wilaya ya Kaliua,Japhael Lufungija,amesema wameokoa muda na maisha ya watoto na wajawazito kwa kutolewa huduma wilayani Kaliua.

 Amesema baadhi ya watoto walikuwa wanapoteza maisha baada ya kuzaliwa kwa kukosa huduma muhimu ambazo hazikuwa zikitolewa kutokana na kukosekana hospitali ya Wilaya.

 Ameongeza kuwa wanaendelea kutenga bajeti ikiwa ni pamoja na kuomba Serikali Kuu ili majengo zaidi na madawa yapatikane na huduma ya mama na mtoto iwe nzuri zaidi.

 Wilaya ya Kaliua iliyoanzishwa mwaka 2014,haikuwa na Hospitali ya Wilaya na wakazi wake zaidi ya laki tatu,kutegemea huduma wilaya ya Urambo na Tabora umbali zaidi ya km 120.

 

Saturday, July 31, 2021

TABORA POLYTECHNIC YATARAJIA KUWA CHUO KIKUU HIVI KARIBUNI


 Robert Kakwesi, Tabora


Taasisi ya vyuo vya ufundi Tabora,Tabora Polytechnic college,kinatarajia kujipanua na kuwa Chuo Kikuu katika muda mfupi ujao.

Mkurugenzi wa Chuo hicho,Shaban Mrutu,alisema wanatambua hakuna Chuo Kikuu katika ukanda wa magharibi wenye mikoa ya Tabora,Katavi,Kigoma na Shinyanga na kuwa  kitakuwa Cha aina yake na mfano.

Akizungumza katika mahafali ya Saba ya Chuo hicho,alisema Chuo kina sifa zote za kupanuka na kuwa Chuo Kikuu ambacho kitatoa fursa kwa Wana Tabora na wakazi wa Kanda ya magharibi ,kunufaika na uwepo wa Chuo hicho kitakachotoa taaluma mbalimbali.

Mrutu pia alisema Wana mpango kuanzia baadae mwaka huu,kujenga hospitali katika Manispaa ya Tabora ambayo itasaidia kutoa huduma ya matibabu kwa wakazi wa Mkoa wa Tabora na hata nje ya mkoa.

"Tuna malengo makubwa ya kusaidia wakazi wa Tabora na mikoa jirani katika sekta za elimu na Afya"Amesema

Amebainisha kuwa wahitimu wa Chuo hicho,wanatoa wakiwa wameiva katika taaluma walizopata na kuwa jamii iwapokee na kuwapa Ushirikiano.

Alitamba kuwa Chuo hicho ni Bora,kikiwa na maabara kubwa na Vifaa vya kisasa yenye uwezo wa kuingiza wanafunzi 250 kwa wakati mmoja na kufanya majaribio.

Mrutu aliongeza kuwa Chuo hicho,kinazingatia Sana kupika wahitimu Bora na ndio maana kundi kubwa limeshindwa kumaliza katika fani mbalimbali.

Mwenyekiti wa bodi ya Chuo hicho,Lucas Ndanga,aliwataka wahitimu kutumia taaluma waliyopata kutoa huduma kwa jamii kwa weledi mkubwa na kujituma.

Ndanga ambaye ni wakili kitaaluma,Alisema muda waliokaa chuoni hapo umewajenga kupambana na maisha katika soko la ajira.

Mkuu wa Wilaya ya Tabora,Dk Yahaya Nawanda,mbali ya kukipongeza Chuo hicho,aliahidi kuwa anamzawadia mwanafunzi Bora Kila mwaka kiasi Cha shilingi laki mbili.

Pia aliahidi kuishawishi Manispaa ya Tabora,nayo kuunga mkono katika kumzawadia mwanafunzi Bora Kila mwaka wa Chuo hicho.


Wahitimu zaidi ya mia mbili na hamsini,wamehitimu katika Chuo hicho katika fani mbalimbali kama afisa tabibu,watunza kumbukumbu na wauguzi.

Monday, June 28, 2021

RC BATILDA ATOA SIKU 2 KUBORESHWA MACHINJIO


Machinjio ya nyama yaliyoko Mtaa wa Kariakoo katika halmashauri ya manispaa Tabora ambayo yanatakiwa kufanyiwa usafi wa kina ili kuboresha mazingira yake. Picha na Allan Ntana.


Na Allan Ntana, Tabora


MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya manispaa ya Tabora Bosco Ndunguru amepewa muda wa siku mbili kuhakikisha machinjio ya nyama yalioko eneo la Kariakoo yanafanyiwa usafi wa kina.


Agizo hilo limetolewa jana na Mkuu wa Mkoa huo Dkt Batilda Buriani alipotembelea na kukagua mazingura ya machinjio hayo akiambana na Mkuu wa wilaya na viongozi wa halmashauri ya manispaa hiyo.


Alisema hali ya usafi katika machinjio hayo hairidhishi, sakafu, kuta na mifereji ya kutolea uchafu ni vichafu sana na vyombo vya kuhifadhia nyama navyo haviridhishi ikiwemo uchakavu wa miundombinu.


Alisema lengo la kujengwa machinjio hayo ni kuongeza vyanzo vya mapato lakini kwa hali ilivyo sasa malengo hayo hayawezi kufikiwa tena hivyo akaagiza maboresho makubwa yafanyike ikiwemo kuanzisha vyanzo vingine vya mapato.


RC Batilda alimtaka Mkurugenzi kutoridhika na mapato wanayopata sasa bali wafanye kila linalowezekana ili kuhakikisha lengo la machinjio hayo kuwa kitovu cha kusafirisha nyama katika mataifa jirani ya Burundi na Rwanda linatimizwa.


‘Fanyeni usafi wa kina, nawapa siku 2 tu mandhari ya machinjio haya yabadilike, pakeni rangi kuta zote, wekeni marumaru (tiles) na maboksi yote ya kuwekea nyama yawe safi, sitaki mniangushe’, alisema RC.


Aliwataka kutumia sehemu ya mapato wanayokusanya kuboresha eneo hilo wakati wakisubiri mradi mkubwa wa Benki ya Dunia ambao utahusisha pia ujenzi wa machinjio hayo kwa kiwango cha kisasa.


Mkuu wa wilaya ya Tabora Mjini Dkt Yahaya Nawanda alimhakikishia kuwa atafanyia kazi maelekezo yote aliyoyatoa haraka iwezekanavyo ili kuhakikisha machinjio hayo yanakuwa na mwonekano mzuri ili kuongeza mapato.


Awali akitoa taarifa, Mkurugenzi Ndunguru alisema kuwa machinjio hayo yaliyojengwa kwa ufadhili wa Jumuiya ya Kiuchumi ya Ulaya (European Economic Community) mwaka 1972 yanakabiliwa na changamoto kubwa ya uchakavu wa miundombinu hali inayosababisha usafi kutoridhisha.



Sunday, May 2, 2021

UJUMBE KUTOKA KWA BALOZI WA SWEDEN TANZANIA KWA UMOJA WA KLABU ZA WAANDISHI WA HABARI MIKOA YOTE TANZANIA TAREHE 3 MEI 2021



Habari za leo, Mimi kama Balozi wa Sweden ninafurahi kuwepo leo kusherekea uhuru wa habari na kujieleza. Sweden na Tanzania ni marafiki wa siku nyingi, na wote tunatambua kwamba nguzo hii, sambamba na haki ya kupata taarifa ni muhimu sana kwa jamii inayoheshimu Demokrasia na Haki za Binadamu. Sweden inaamini kwamba maendeleo ya nchi yoyote ile yanapatikana kwa kupeana tarifa, kujadiliana kwa uwazi, na kuwajibishana. Basi sisi tutaendelea kuungana na watanzania wote katika jitihada za kukuza na kuendeleza uhuru wa habari na kujieleza nchini. Asanteni sana kwa kunisikiliza 

Saturday, May 1, 2021

WAKULIMA WA TUMBAKU KAHAMA WATARAJIA KUJIPATIA BILION AROBAINI

Wakulima wa Tumbaku wa wilaya ya Kahama wamekuwa wa kwanza kufungua milango ya soko la kuuza tumbaku yao kwenye makampuni  huko mjini Tabora huku wakitarajia kupata zaidi ya shilingi Bilion arobaini kutokana na mauzo ya zao hilo kwa kilo milioni tisa walizoingia mkataba na Makampuni yanayonunua Tumbaku nchini.

Wednesday, April 21, 2021

TUNAOMBA MSAADA WA UJENZI WA MSIKITI

WAISLAM TABORA WAOMBA MSAADA.

Waislam katika msikiti wa Ijumaa Ikindwa kata ya Kiloleni Manispaa ya Tabora wameshindwa kukamilisha ujenzi wa msikiti huo kwa kile kinachoelezwa kukosa uwezo wa kifedha wa kumalizia msikiti huo ambao unahitaji zaidi ya shilingi million tano.

Sunday, April 18, 2021

PROF. GABRIEL AAGIZA UZALISHAJI WA CHANJO YA UGONJWA WA MIGUU NA MIDOMO MWAKANI!

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel akizungumza na baraza la wafanyakazi la Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) jijini Dar es Salaam na kuitaka TVLA kuhakikisha mwaka ujao inazalisha chanjo ya mifugo ya ugonjwa wa miguu na midomo (FMD) ili bidhaa zitokanazo na mifugo ziweze kupata masoko ya kimataifa. (Picha na Edward Kondela)

 


Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Hezron Nonga akizungumza na baraza la wafanyakazi la Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) jijini Dar es Salaam (hawapo pichani) na kukiarifu kikao hicho kuwa mkakati uliopo ni kuhakikisha mwaka ujao zinazalishwa chanjo tatu za mifugo ikiwemo ya kichaa cha mbwa ili kufikia ukomo wa ugonjwa huo. (Picha na Edward Kondela)

Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Dkt. Stella Bitanyi akizungumza kwenye baraza la wafanyakazi la TVLA na kubainisha kuwa tayari wamezalisha chanjo ya saba ya homa ya mapafu ya mbuzi kati ya chanjo 13 za kimkakati na imethibtishwa na maabara ya chanjo za mifugo Afrika na imepata cheti cha ubora na uzalishaji wake umeshaanza. (Picha na Edward Kondela)

 


Wajumbe wa baraza la wafanyakazi la Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) wakisikiliza hoja mbalimbali kutoka kwa viongozi wao (hawapo pichani) akiwemo mgeni rasmi aliyefungua kikao cha baraza hilo Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel. Kikao kimefanyika katika ukumbi wa TVLA jijini Dar es Salaam. (Picha na Edward Kondela)

Picha ya pamoja ya mgeni rasmi Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel baada ya kufungua kikao cha baraza la wafanyakazi la Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) jijini Dar es salaam. (Picha na Edward Kondela)

  


 Na. Edward Kondela

 

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel ameagiza upatikanaji wa chanjo ya mifugo ya ugonjwa wa miguu na midomo (FMD) ifikapo mwakani ili bidhaa zitokanazo na mifugo ziweze kuuzwa katika masoko ya kimataifa.

Prof. Gabriel ameyasema hayo jana (16.04.2021) jijini Dar es Salaam wakati akifungua kikao cha baraza la wafanyakazi la Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA), ambapo amemuelekeza Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo Prof. Hezron Nonga kusimamia utekelezaji wa uanzishwaji wa chanjo hiyo ili kuwezesha viwanda vinavyozalisha nyama zitokanazo na mifugo hapa nchini kupata masoko ya bidhaa zao katika nchi mbalimbali.

Aidha ameitaka TVLA kuhakikisha changamoto ya homa ya nguruwe inatatuliwa kwa kupatikana kwa chanjo yake na kutokomeza kabisa ugonjwa huo hapa nchini na kuondoa dhana iliyojengeka kwa baadhi ya wananchi kuwa baadhi ya mifugo imekuwa ikibaguliwa katika upatikanaji wa huduma mbalimbali zikiwemo za chanjo. 

Naye Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Hezron Nonga amesema mkakati uliopo ni kuhakikisha mwaka ujao zinazalishwa chanjo tatu za mifugo ikiwemo ya kichaa cha mbwa ili kufikia ukomo wa ugonjwa huo kwa kuwa lengo la dunia ni kuhakikisha ifikapo mwaka 2030 ugonjwa huo unatokomezwa duniani.

Pia amesema chanjo zingine za ugonjwa wa sotoka ya mbuzi na kondoo tayari hatua zaidi zinaendelea kufanywa na TVLA ili kuhakikisha mwaka ujao chanjo hizo zinazalishwa hapa nchini pamoja na kuzalisha chanjo ya mapele ngozi. 

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Dkt. Stella Bitanyi amesema wakala hiyo tayari imezalisha chanjo ya saba ya homa ya mapafu ya mbuzi kati ya chanjo 13 za kimkakati na tayari imethibtishwa na maabara ya chanjo za mifugo Afrika na imepata cheti cha ubora na uzalishaji wake umeshaanza. 

Dkt. Bitanyi amesema TVLA inatategemea kuzindua chanjo hiyo kati ya Mwezi Mei na Juni mwaka huu ili itangazwe na wafugaji waanze kuitumia pamoja na kuweka mikakati ya uwezo wa kuzalisha zaidi chanjo dhidi ya homa ya mapafu ya ng’ombe kwa kuagiza mashine yenye uwezo mkubwa zaidi wa kuzalisha chanjo hiyo.

Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) ambayo ipo chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi inafanya jitihada mbalimbali kuhakikisha inazalisha chanjo 13 za mifugo ambazo ni za kimkakati.

Thursday, April 15, 2021

TASAF YANUFAISHA WATOTO 6,704 KIELIMU IGUNGA



 

Na Allan Ntana, Igunga

 

JUMLA ya watoto 6,704 kutoka katika familia za kaya maskini 4,766 zinazonufaika na mpango wa kunusuru kaya maskini (TASAF) wilayani Igunga Mkoani Tabora zimewezeshwa kupata elimu na mahitaji yote ya shuleni.

 

Hayo yamebainishwa jana na Mratibu Msaidizi wa TASAF wilayani humo Richard Elias Mtamani alipokuwa akitoa taarifa ya utekelezaji mpango huo kwa waandishi wa habari waliokwenda kutembelea miradi iliyoanzishwa na kaya hizo.

 

Alisema kuwa mpango huo ulioanza kutekelezwa mwaka 2015 wilayani humo umeshanufaisha jumla ya kaya maskini 4,766 katika vijiji 54 na hadi sasa wameshawezeshwa jumla ya sh bil 5.3 na wanaendelea kupokea ruzuku hiyo.

 

Alibainisha kuwa kupitia mpango huo jumla ya watoto 6,704 kutoka katika kaya hizo wamenufaika kwa kupelekwa shule za msingi na kununuliwa mahitaji yao yote ya kielimu ikiwemo viatu, sare za shule, madaftari na kalamu.

 

Mtamani alifafanua kuwa mbali na watoto hao ambao husomeshwa katika shule za msingi na sekondari wilayani humo pia watoto 1,913 wenye umri chini ya miaka 5 wamenufaika na huduma za afya kwa kupelekwa kliniki.

 

Mtendaji wa Kijiji cha Migongwa katika kata ya Mwamashiga wilayani humo Saida Sagwa Nkuba alipongeza mpango huo wa serikali kwa kuwezesha watoto wanaotoka katika kaya maskini kupata elimu.

 

‘Hawa watoto wanafanya vizuri sana darasani, mwaka jana Suzana Daudi aliyekuwa darasa la 7 katika shule ya msingi Migongwa aliongoza kwa ufaulu katika shule zote 4 za kata hiyo na sasa anasoma Mwamashiga sekondari’, alisema.

 

Mwalimu Mkuu wa shule ya msingi Migongwa, Nkuba Shadi Malambo, alisema kuwa kitendo cha watoto hao kupewa mahitaji yao yote ya shule kimewahamasisha kupenda shule na kujituma katika masomo yao na sasa wanafanya vizuri sana.

 

Alieleza kuwa awali watoto hao walishindwa kuja shule kutokana na umaskini wa wazazi wao ikiwemo umbali mrefu kutoka wanakoishi hadi shuleni lakini baada ya familia zao kuanza kuwezeshwa na TASAF mahudhurio na ufaulu vimeongezeka.

 

Alitoa mfano wa matokeo ya mwaka jana ya darasa la 7 katika shule hiyo ambapo watoto 37 kati ya 43 walichaguliwa kwenda sekondari huku watoto 12 wa darasa hilo kutoka kaya maskini wakifaulu wote. 

 

Mtoto Suzane James (15) wa darasa la 6 katika shule hiyo alisema kuwa kabla ya wazazi wao kuingizwa katika mpango huo walikuwa wanashinda njaa na hawakuwa na viatu wala sare za shule jambo lililowakwamisha kuja shule.

 

SERIKALI YAZINDUA MRADI WA REA III (AWAMU YA 2) ....KUTUMIA SH TRIL 1.3 KUPELEKA UMEME VIJIJI VYOTE NCHINI




Na Allan Ntana, Tabora

 

SERIKALI imezindua mradi kabambe wa kusambaza Umeme Vijijini (REA Awamu ya 3 Mzunguko wa Pili ambao utafikisha nishati hiyo katika vijiji vyote ambavyo vilikuwa havijafikiwa na huduma hiyo katika mikoa na wilaya zote hapa nchini.

 

Akizungumza katika uzinduzi huo uliofanyika jana kitaifa katika kijiji cha Ugaka kata ya Ugaka, Jimbo la Manonga wilayani Igunga Mkoani Tabora, Waziri wa Nishati Dkt Medard Matogoro Kalemani alisema kuwa mradi huo wa kipekee utatekelezwa katika vijiji, vitongoji na mitaa yote hapa nchini ndani ya miezi 18.

 

Alisema kuwa mradi huo unaofadhiliwa na serikali ya awamu ya tano ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Benki ya Dunia utateketekelezwa na Wakandarasi 3 kwa gharama ya zaidi ya sh tril 1.2.

 

Alibainisha kuwa hadi kufikia Desemba mwaka jana zaidi ya vijiji 10,188 kati ya  12,268 vilivyoko hapa nchini vilikuwa vimeunganishiwa nishati hiyo chini ya usimamizi wa Wakala wa Umeme Vijijini (REA) na sasa vimebakia vijiji 1, 974 tu ambavyo vitaunganishiwa kupitia awamu hii.

 

‘Serikali inayoongozwa na Rais Dkt John Pombe Magufuli imedhamiria kufikisha umeme wa REA katika vijiji, vitongoji na mitaa yote ikiwemo taasisi za umma, hivyo akatoa wito kwa wananchi wote kuchangamkia fursa hiyo’, alisema.

 

Waziri Kalemani alifafanua kuwa tangu kuanza kwa mradi huo wa usambazaji umeme vijijini (REA) awamu ya 1, 2 na 3 hadi sasa serikali imetumia jumla ya sh tril 3.8 na kusisitiza kuwa hawataruka kijiji, kitongoji wala mtaa wowote.

Ili kutimiza lengo la serikali la kufikisha huduma hiyo katika vijiji, vitongoji na mitaa yote isiyo na umeme hapa nchini aliwataka Wakandarasi waliopewa kazi hiyo kuimaliza kwa wakati na kuonya kuwa yeyote atakayezembea atawajibishwa.

 

Aidha aliwataka Mameneja na Wataalamu wa Shirika la Umeme nchini TANESCO kufungua ofisi za muda katika vijiji vyote ili kuepusha usumbufu wa wananchi (wateja) kusafiri umbali mrefu kwenda wilayani kulipia huduma hiyo.

 

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya REA Julius Bundala aliahidi kusimamia ipasavyo utekelezaji mradi huo ili kutimiza azma ya serikali ya kufikisha nishati hiyo katika vijiji vyote hapa nchini.

 

Katibu wa CCM Mkoa wa Tabora Solomon Kasaba alisema kuwa mradi huo ni fursa muhimu sana ya kiuchumi kwa wakazi wa vijijini hivyo akawataka kuanzisha viwanda vidogo, saluni na miradi ya uchomeleji vyuma ili kujikwamua kimaisha.

 

Naye Mkuu wa Mkoa huo Dkt Philemon Sengati alibainisha kuwa serikali imewatendea haki wakazi wa mkoa huo kwani kati ya vijiji 724 vya mkoa huo vijiji 377 vimeshaunganishiwa huduma hiyo na vilivyobaki vitapata huduma hiyo ndani ya miezi 18 tu.

 

 

Wednesday, April 14, 2021

WAFANYABIASHARA WAONYWA KUACHA KUTOROSHA MIFUGO NJE YA NCHI!

 

Na. Edward Kondela


 

Wafanyabiashara wa mifugo nchini wametakiwa kuepuka kusafirisha mifugo yao kwenda nje ya nchi bila kufuata utaratibu kwa kuwa serikali itakosa mapato kupitia rasilimali za nchi na pia ni kosa kisheria.

 

Akizungumza jana (14.04.2021) wakati alipotembelea eneo ambalo Wizara ya Mifugo na Uvuvi imepewa na Kijiji cha Horohoro Kijijini, kilichopo Wilaya ya Mkinga Mkoani Tanga, kwa ajili ya kuanzisha mnada wa mifugo wa mpakani, Katibu Mkuu wa wizara hiyo anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel amesema wizara haitakuwa tayari kumtetea mfanyabiashara yeyote atakayebainika kutenda kosa hilo.

 

Prof. Gabriel amesema Wizara ya Mifugo na Uvuvi imedhamiria kuanzisha mnada wa mpakani kati ya Tanzania na Kenya katika Kijiji cha Horohoro Kijijini kabla ya mwaka ujao wa fedha 2021/22 ili kudhibiti baadhi ya wafanyabiashara ambao wamekuwa wakitorosha mifugo kwenda nchi ya jirani kwa ajili ya kuuza.

 

“Mfanyabiashara akibainika kufanya hivyo atashughulikiwa kwa kutumia mkono wa sheria, kwani kwa kufanya hivyo inakosesha serikali mapato kupitia rasilimali za nchi.” Amefafanua Prof. Gabriel

 

Ameongeza kuwa eneo hilo ambalo wizara imepatiwa na Kijiji cha Horohoro Kijijini lina ukubwa wa ekari 23 na lipo kando mwa barabara kuu ya kuelekea mpakani mwa Tanzania na Kenya, hivyo uwepo wa mnada huo utawezesha wafugaji wa Tanzania kuuza mifugo yao kwa wafanyabishara wa nchi hizo mbili.

 

Ametoa wito kwa wafugaji Mkoa wa Tanga na mikoa ya jirani kuwa malighafi ya biashara ya minada ni mifugo, hivyo watambue jitihada za serikali na kumnukuu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan ambaye ameitaka Sekta ya Mifugo kusogeza huduma zinazotakiwa kwa wafugaji ili mifugo yao isikonde na wafugaji wasikonde kiuchumi.

 

Aidha, amebainisha kuwa nia ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi ni kuhakikisha Sekta ya Mifugo inachangia zaidi katika pato la taifa hivyo ni lazima kudhibiti utoroshaji wa mifugo kwenda nchi za jirani.

 

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Horohoro Kijijini Bw. Jumapili Yohana amesema wameamua kuipatia Wizara ya Mifugo na Uvuvi eneo hilo bila malipo yoyote wakiamini uwepo wa mnada mpakani katika kijiji hicho kutachangia kwa kiasi kikubwa kuongeza ajira na kukuza biashara zingine ikiwemo ya vyakula.

 

Bw. Yohana amesema kijiji kimefuata taratibu zote za ardhi na kukubaliana kuwa mara baada ya mnada huo utakapoanza kufanya kazi utachangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya kijiji chao na kuishukuru wizara kwa ushirikiano.

 

Pia, Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Mifugo Prof. Elisante Ole Gabriel akiwa katika ziara ya siku moja Mkoani Tanga amefika Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) na kujionea shughuli mbalimbali ikiwemo ya tafiti ya malisho bora ya mifugo na kuwaasa wafugaji kuipatia mifugo yao malisho bora ili iweze kuwa na afya njema na kuwa na nyama bora, maziwa bora na ngozi bora.

 

Amewataka wafugaji kufuga kisasa kwa kutumia sayansi na kuitaka TALIRI kusambaza tafiti zao mikoa mbalimbali ili wafugaji waweze kupata elimu ya kufuga kisasa na kuwa na mifugo bora na yenye afya ambayo itakuwa na tija kiuchumi.

 

Amewaasa pia wawekezaji na watu wanaofikiria kuwekeza, wafikirie kuwekeza katika malisho ya mifugo ili malisho bora yapatikane kwa wingi kwa kuwa wafugaji wengi wameanza kubadili fikra za ufugaji na kuhitaji malisho ya kisasa na kisayansi ambayo yanafaa kwa matokeo chanya ya mifugo yao.

 

Prof. Gabriel katika ziara yake ya siku moja Mkoani Tanga ametembelea pia Ranchi ya Mzeri iliyopo Wilaya ya Handeni na kuzungumza na wawekezaji waliopatiwa vitalu katika ranchi hiyo na Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) na kukemea tabia ya baadhi ya watu wanaoiba mifugo kwenye maeneo mbalimbali nchini ikiwemo kwenye ranchi.

 

Katibu mkuu huyo pia amefika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga na kuwa na mazungumzo na mkuu wa mkoa huo Mhe. Martine Shigella pamoja na Katibu Tawala wa mkoa Bi. Judica Omari juu ya maendeleo ya sekta ya mifugo katika Mkoa wa Tanga.

 

RC SENGATI AKUNWA UBORA WA MIRADI YA MAJI TABORA

 


 

Na Allan Ntana, Tabora

 

MKUU wa Mkoa wa Tabora Dkt Philemon Sengati ameleezea kufurahishwa na ubora wa miradi ya maji iliyotekelezwa na Wakala wa Usambazaji Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Mkoani hapa katika vijijini mbalimbali.

 

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama uliotekelezwa katika kijiji cha Migungumalo kata ya Usagari wilayani Uyui juzi alimpongeza Meneja wa RUWASA Mkoa kwa usimamizi bora wa miradi.

 

Alisema kuwa miradi iliyotekelezwa na inayoendelea kutekelezwa katika maeneo mbalimbali Mkoani humo imeongeza kiwango cha upatikanaji huduma ya maji safi na salama kwa wakazi wa vijijini kutoka asilimia 30 hadi 70.

 

‘Nimeridhishwa na utendaji wa RUWASA katika Mkoa huu, endeleeni hivi hivi, naamini miradi hii na ule wa ziwa Victoria uliogharimu zaidi ya sh bil 600 itamaliza kero ya maji katika wilaya zote 7 za mkoa wetu’, alisema.

 

Sengati alibainisha kuwa weledi na ufanisi mkubwa wa wataalamu hao umewezesha mkoa huo kuongoza nchi nzima katika utekelezaji miradi ya maji iliyogharamiwa na mradi wa P4R.

 

Alifafanua kuwa mahitaji ya maji katika mkoa huo ni lita za ujazo mil 37 wakati yaliyozalishwa kutokana na mradi mkubwa wa ziwa Victoria ni lita mil 54 hivyo kuufanya mkoa huo kuwa na maji mengi kuliko watumiaji kwa maeneo ya mjini.

 

Alieleza kuwa huduma ya maji safi na salama imeboreshwa kwa kiasi kikubwa katika mkoa huo kutokana na usimamizi bora wa miradi iliyotekelezwa hivyo akatoa wito kwa wageni kuja kujifunza kupitia miradi hiyo.

 

 

Aidha aliongeza kuwa kuboreshwa kwa huduma ya maji katika vijiji mbalimbali mkoani humo kutafanya watu wengi kuwa wasafi hivyo kuongeza kasi ya kuzaliana.

 

Sengati aliwataka wakazi wa mkoa huo kujiepusha na vitendo vya uharibifu wa mazingira ili kulinda na kutunza vyanzo vya maji vilivyopo.

 

Meneja wa RUWASA Mkoani humo Mhandisi Hatari Kapufi alisema kuwa hadi kufikia Machi 2020 wakazi 1,479,750 kati ya 2,390,039 waishio vijijini walikuwa na uwezo wa kupata huduma ya maji safi kwa asilimia 62.4 kwa baadhi ya maeneo asilimia imeongezeka hadi 70.

 

Alibainisha kuwa RUWASA imeweza kutekeleza miradi mbalimbali mkoani humo kupitia programu za PbR, P4R na Mfuko wa Maji (NWF) na hadi kufikia Machi 30 mwaka huu miradi mingi inatarajiwa kukamilika.

 

Aliongeza kuwa kupitia mpango huo jumla ya miradi 31ya maji yenye thamani ya zaidi ya sh bilioni 8.7 imetekelezwa katika mkoa huo na baadhi imekamiilka na mingine iko katika hatua za mwisho.

 

Kwa upande wake Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Kaliua Mkoani hapa Salome Luhingulanya alisema kuwa serikali ya CCM inawajali sana wananchi wake hivyo akawataka wakazi wa mkoa huo kutumia vizuri miradi hiyo.

Wednesday, March 24, 2021

KAMATI SIASA CCM TABORA YATETEA WAKANDARASI WAZAWA

 Robert Kakwesi, Tabora


Kamati ya siasa Mkoa wa Tabora,CCM, imeiomba Serikali kutoa kipaumbele kwa Wakandarasi wazawa katika eneo husika kwenye miradi ya ujenzi pindi inapotangazwa ili kuwaimarisha kimitaji na uwezo na kuimarisha uchumi wa eneo husika.

Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tabora kwa niaba ya Chama chake,Hassan Wakasuvi, wakati alipoongoza  wajumbe wenzake Kamati ya Siasa kukagua ujenzi wa  barabara ya Urambo hadi Kaliua,yenye urefu wa Km  28 iliyojengwa na Kampuni ya Samota..

Alisema Wakandarasi wazawa ambao wanaonyesha uwezo na uaminifu katika utekelezaji wa miradi ikiwemo ya ujenzi wa barabara pindi zabuni zinapotangazwa na wao kuomba, wapewe upendeleo kwa ajili ya kuwajenga na kuwaimarisha zaidi ili wakue na kuweza nao kuomba kazi nje ya Nchi.

Hatua hii itasaidia kupunguza gharama ya mradi kwa Serikali kwa kuwa Mkandarasi wa eneo husika hatakuwa na gharama kubwa za usafishaji wa mitambo kutoka mbali"Alisema

Mwenyekiti huyo alitoa wito kwa viongozi wa CCM kuanzia ngazi ya Shina hadi Mkoa na wananchi wote kuwa walinzi wa miundombinu inayojengwa kwa kuwafichua wezi wa alama za barabara ili iweze kuwa rafiki kwa watumiaji.

Alisema kung’oa  alama hizo kumekuwa kukirudisha nyuma juhudi kubwa za Serikali na kuongeza lazima wahalifu wafichuliwe na kuchukuliwa hatua kali ili kudhibiti uovu huo.

Mkurugenzi wa Kampuni ya Samota,Salumu Abdallah aliishukuru Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuwaamini wazawa na kuwapatia miradi ya ujenzi wa barabara kubwa ikiwemo wao ambao wanajenga barabara ya kutoka Urambo hadi Kaliua kwa gharama ya Sh38.7bilioni.

Alisema hatua hiyo imewasaidia sana kuwajengea uwezo na kupata ujuzi kutoka Mshauri Msimamizi ambapo hivi sasa wana uwezo wa kufanya kazi nyingine kubwa za ujenzi wa barabara kutokana mafunzo wanayopata.

Abdallah alisema ni vema Serikali inapokuwa na miradi ikaweka utaratibu wa kutenga miradi ambayo wazawa wanapaswa kujenga kwa kuwa wao hawana uwezo wa kushindana kwenye zabuni na Kampuni za nje ya Nchi kutokana na mitaji yao kuwa midogo ukilinganisha na wageni.

Meneja wa Mkoa wa Tabora wa Wakala wa Barabara Nchini ,Tanroads, Damian Ndabalinze, alisema barabara hiyo ya kutoka Urambo hadi Kaliua imekamilika kwa kiwango kikubwa zilizobaki ni kazi ndogo ndogo ambazo zinatarajiwa kumalizika mwishoni mwa mwezi huu.

Alisema baadhi ya shughuli zilizobaki ni pamoja na mifereji ya maji ya mvua, kuweka alama za kuvuka watu, kuweka mawe yanayoonyesha umbali, na kuchora michoro ya usalama barabarani .