Featured Post

HALMASHAURI KALIUA YATOA MIKOPO SHILINGI MILIONI 240

MATANGAZO

Monday, June 28, 2021

RC BATILDA ATOA SIKU 2 KUBORESHWA MACHINJIO


Machinjio ya nyama yaliyoko Mtaa wa Kariakoo katika halmashauri ya manispaa Tabora ambayo yanatakiwa kufanyiwa usafi wa kina ili kuboresha mazingira yake. Picha na Allan Ntana.


Na Allan Ntana, Tabora


MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya manispaa ya Tabora Bosco Ndunguru amepewa muda wa siku mbili kuhakikisha machinjio ya nyama yalioko eneo la Kariakoo yanafanyiwa usafi wa kina.


Agizo hilo limetolewa jana na Mkuu wa Mkoa huo Dkt Batilda Buriani alipotembelea na kukagua mazingura ya machinjio hayo akiambana na Mkuu wa wilaya na viongozi wa halmashauri ya manispaa hiyo.


Alisema hali ya usafi katika machinjio hayo hairidhishi, sakafu, kuta na mifereji ya kutolea uchafu ni vichafu sana na vyombo vya kuhifadhia nyama navyo haviridhishi ikiwemo uchakavu wa miundombinu.


Alisema lengo la kujengwa machinjio hayo ni kuongeza vyanzo vya mapato lakini kwa hali ilivyo sasa malengo hayo hayawezi kufikiwa tena hivyo akaagiza maboresho makubwa yafanyike ikiwemo kuanzisha vyanzo vingine vya mapato.


RC Batilda alimtaka Mkurugenzi kutoridhika na mapato wanayopata sasa bali wafanye kila linalowezekana ili kuhakikisha lengo la machinjio hayo kuwa kitovu cha kusafirisha nyama katika mataifa jirani ya Burundi na Rwanda linatimizwa.


‘Fanyeni usafi wa kina, nawapa siku 2 tu mandhari ya machinjio haya yabadilike, pakeni rangi kuta zote, wekeni marumaru (tiles) na maboksi yote ya kuwekea nyama yawe safi, sitaki mniangushe’, alisema RC.


Aliwataka kutumia sehemu ya mapato wanayokusanya kuboresha eneo hilo wakati wakisubiri mradi mkubwa wa Benki ya Dunia ambao utahusisha pia ujenzi wa machinjio hayo kwa kiwango cha kisasa.


Mkuu wa wilaya ya Tabora Mjini Dkt Yahaya Nawanda alimhakikishia kuwa atafanyia kazi maelekezo yote aliyoyatoa haraka iwezekanavyo ili kuhakikisha machinjio hayo yanakuwa na mwonekano mzuri ili kuongeza mapato.


Awali akitoa taarifa, Mkurugenzi Ndunguru alisema kuwa machinjio hayo yaliyojengwa kwa ufadhili wa Jumuiya ya Kiuchumi ya Ulaya (European Economic Community) mwaka 1972 yanakabiliwa na changamoto kubwa ya uchakavu wa miundombinu hali inayosababisha usafi kutoridhisha.



No comments:

Post a Comment