Featured Post

HALMASHAURI KALIUA YATOA MIKOPO SHILINGI MILIONI 240

MATANGAZO

Saturday, December 26, 2020

WADAIWA SUGU WA MAPATO MANISPAA TABORA KUSAKWA

Meya wa Halmashauri ya Manispaa Tabora Ramadhani Kapela (aliyeketi katikati) akimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa manispaa hiyo Bosco Ndunguru katika kikao cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo kiichofanyika hivi karibuni katika manispaa hiyo. Picha na Allan Ntana.
 



Na Allan Ntana, Tabora


HALMASHAURI ya manispaa Tabora inatarajia kuendesha msako maalumu kwa wadaiwa sugu wa mapato yatokanayo na ushuru ili kila mmoja alipe madeni yake, na watakaoshindwa kulipa watachukuliwa hatua za kisheria.


Hayo yamebainishwa juzi na Mkuu wa wilaya ya Tabora Mjini ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya hiyo Komanya Erick Kitwala alipokuwa akiongea na gazeti hili ofisini kwake.


Alisema kuwa licha ya wadaiwa hao kutakiwa kulipa madeni yao kwa wakati au kupunguza hadi watakapomaliza baadhi yao wamekuwa wakikwepa na wengine kutotoa ushirikiano jambo linalopelekea halmashauri kukosa mapato.


Alisisitiza kuwa mapato ya halmashauri ndiyo yanayofanikisha utekelezaji miradi ya maendeleo ya wananchi, hivyo hawezi kukubali watu waendelee kulimbikiza madeni tu pasipo kulipa.


Kitwala alibainisha kuwa baadhi ya watendaji wamekuwa hawatekelezi wajibu wao ipasavyo kwa kutofuatilia na kuchukua hatua stahiki kwa wale wote wanaokwepa kulipa mapato ya serikali, huku akionya kuwa Mtendaji yeyote atakayebainika kuwa chanzo cha upotevu wa mapato hayo atawajibika.


‘Tutafanza oparesheni maalumu ya kukusanya madeni kwa wadaiwa sugu wote katika maeneo mbalimbali ya manispaa, naomba kila mdaiwa sugu ajisalimishe mapema na kulipa deni lake kabla ya kuchukuliwa hatua ’, alisema.


Kwa upande wake Meya wa Manispaa hiyo Ramadhan Kapela alisema kuwa mapato mengi yamekuwa yakipotea kutokana na baadhi ya Watendaji wasio waaminifu na kutowajibika ipasavyo, hivyo akawataka kubadilika mara moja.


Alibainisha kuwa madiwani wana dhamana kubwa ya kusimamia mapato ya halmashauri hivyo akawataka kufuatilia zoezi la ukusanyaji mapato kwa Watendaji wa vijiji na kata ili watekelekeze wajibu ipasavyo.


Alibainisha kuwa miradi mingi inayotekelezwa na serikali inashindwa kukamilika kwa wakati kutokana na ufinyu wa bajeti, hivyo akawataka kuongeza kasi ya ukusanyaji mapato ikiwemo kufuatilia madeni yote ili yalipwe.


Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Tabora mjini Emanuel Mwakasaka aliwataka madiwani hao kuwa kitu kimoja na kuhakikisha mapato ya serikali yanayokusanywa yanatumika ipasavyo.


Aidha alishauri wale wote watakaobainika kukwepa kulipa kodi hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yao ili kuwezesha miradi mingi zaidi kutekelezwa ikiwemo kuwezesha vikundi vyote vya vijana, walemavu na akinamama wajasiriamali.


KANISA LA KCC LAMPONGEZA RAIS MAGUFULI


 Kwaya ya Wanaume (CMF) ya kanisa la TAG Kitete Christian Center lililopo katika manispaa ya Tabora wakiimba katika ibada maalumu ya Krismas iliyofanyika katika kanisa hilo. Picha na Allan Ntana.



Na Allan Ntana, Tabora


KANISA la TAG-Kitete Christian Center lililopo katika manispaa ya Tabora limempongeza Rais Dkt.John Pombe Magufuli kwa kumtanguliza Mungu katika utawala wake na kuliwezesha taifa kuvuka salama katika kipindi kigumu cha ugonjwa wa COVID 19.


Pongezi hizo zimetolewa jana na Askofu Mstaafu ambaye pia ni Mchungaji Kiongozi wa kanisa hilo Rev. Paul Meivukie katika ibada ya sikukuu ya Krismas iliyofanyika jana kanisani hapo.


Alisema kuwa katika sikukuu hii ya kuzaliwa Yesu Kristo jamii inapaswa kumshukuru Mungu kwa mambo makubwa aliyoyafanya katika taifa letu na kwa jinsi alivyomwongoza Rais Magufuli katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa homa kali ya mapafu (covid-19).


Alisema kuwa mioyo ya Watanzania wote inabubujika shukrani kwa Mungu kwa jinsi Rais wetu alivyosimama katika imani na kutangaza maombi ya siku 3 ya nchi nzima kuomba dua na sala na Mungu akasikia kilio chetu na kuliponya taifa.


Kwa upande wake Mchungaji Msaidizi wa kanisa hilo Rev Shadrack Herman aliwataka Watanzania kuendelea kumtumaini Yesu Kristo na kumpa nafasi katika maisha yao ili awalee na kuwapitisha katika magumu yote wasiyoyaweza.


Baadhi ya waumini wa kanisa hilo Dkt. Zefania Zenga, Jovent William, Peter Seme na Andrew Sebastian walisema kuwa Rais Magufuli ni kiongozi na mtumishi wa Mungu, imani yake imelibeba taifa na kuokoa roho za wananchi.


Walibainisha kuwa kama sio ujasiri na imani aliyonayo kwa Mungu ugonjwa wa corona usingeisha haraka kiasi hicho na watu wengi wangepoteza maisha kama inavyotokea katika mataifa mengine.


Walibainisha kuwa Mungu ni mweza wa yote hivyo wakaitaka jamii kuendelea kumtumaini katika kila jambo ili aendelee kutenda makuu ikiwemo kudumishwa amani, upendo na mshikamano hapa nchini.


Aidha waliitaka jamii kuendelea kuchukua tahadhari ya ugonjwa wa corona kwa kunawa mikono mara kwa mara huku wakisisitiza kumtanguliza Mungu katika kila jambo.


Aidha waliwataka waumini wa madhehebu yote ya dini kuendelea kumwombea Rais Magufuli na wasaidizi wake ili waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo na  kuharakisha maendeleo ya wananchi.

Monday, December 21, 2020

MADIWANI KALIUA WATAKIWA KUIGA KASI YA UTENDAJI WA JPM


 Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Kaliua Mkoani Tabora Raphael Lufungija (wa tatu kutoka kulia) akiongoza madiwani wenzake wa halmashauri ya wilaya hiyo kula kiapo cha uadilifu katika kikao cha baraza hilo kilichofanyika juzi wilayani humo. Picha na Allan Kitwe.



Na Allan Kitwe, Kaliua


MADIWANI wa halmashauri ya wilaya ya Kaliua Mkoani Tabora wametakiwa kuiga kasi ya utendaji wa Rais Dkt John Pombe Magufuli kwa kutekeleza wajibu wao kwa weledi mkubwa ili kuharakisha maendeleo ya wananchi wa kata zao.


Rai hiyo imetolewa juzi na Katibu Tawala wa wilaya hiyo Michael Nyahinga katika kikao cha kwanza cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo kilichoketi kwa ajili ya kumchagua Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa halmashauri hiyo.


Alisema kuwa kasi na weledi wa Rais Magufuli ni kielelezo kizuri sana kwa kiongozi yeyote yule anayetaka mafanikio, hivyo akawataka madiwani hao kutekeleza wajibu wao kwa wananchi kwa vitendo na sio maneno tu. 


Alisisitiza kuwa wananchi wanataka maendeleo na kutatuliwa kero zao na sio kuendekeza malumbano yasiyo na tija katika vikao vya baraza ambavyo ndivyo vyenye mamlaka ya kupitisha mipango ya maendeleo ya wananchi.


‘Nawapongeza madiwani wote mlioshinda katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu, uchaguzi umeisha sasa kila mmoja akatekeleze wajibu wake kwa vitendo na kwa kuzingatia kanuni, taratibu na sheria’, alisema.


Katibu Msaidizi Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Magharibi, Gerald Mwaitebele aliwataka kuzingatia maadili ya utumishi na kujiepusha kumiliki mali za udharimu huku akionya kuwa yeyote atakayeenda kinyume na kiapo hicho atachukuliwa hatua za kisheria.


Naye Mwenyekiti mpya wa halmashauri hiyo Japhael Lufungija ambaye ni diwani wa kata ya Ilege (CCM) aliahidi kusimamia kwa nguvu mapato ikiwemo kuibua  vyanzo vipya ili kuwezesha halmashauri hiyo kutekeleza miradi yake ya maendeleo.


Alisisitiza kuwa watashirikiana na serikali kuu kwa ukaribu zaidi ili miradi yote inayotekeleza kwa fedha za ruzuku au wahisani zitumike ipasavyo huku akionya mtumishi yeyote atakayetumia vibaya fedha hizo atakumbana na mkono wa sheria.


Makamu Mwenyekiti wa halmashauri hiyo Abdallah Hemed (diwani wa kata ya Ufukutwa) alisema ili kupata maendeleo makubwa, madiwani wote wanapaswa kushikamana na kushiriki ipasavyo katika suala zima la ukusanyaji mapato.


Aidha alibainisha kuwa utekelezaji wa ahadi walizotoa kwa wananchi utategemeana sana na kasi ya ukusanyaji mapato, hivyo akatoa wito kwa madiwani na watendaji wote kufanya kazi kama timu moja.



SIKONGE WAKAMATA ZANA HARAMU ZA UVUVI ZENYE THAMANI YA ZAIDI YA MIL 100


 Mkuu wa wilaya ya Sikonge Mkoani Tabora Peresi Magiri (mwenye suti nyeusi) akiwa na viongozi wenzake jana wakati wa zoezi la kuteketeza zana haramu za uvuvi zilizokamatwa na Maofisa wa Idara ya Mifugo na Uvuvi wilayani humo hivi karibuni. Picha na Allan Ntana 


Na Allan Ntana, Tabora


HALMASHAURI ya wilaya ya Sikonge Mkoani Tabora imekamata zana haramu za uvuvi zenye thamani ya zaidi ya sh mil 100 na watu 7 waliokuwa wakijihusisha na vitendo hivyo wanashikiliwa na jeshi la polisi kwa tuhuma za kusababisha uharibifu mkubwa wa viumbe maji.


Akizungumza na vyombo vya habari jana Mkuu wa wilaya hiyo Peresi Magiri alipongeza halmashauri hiyo kupitia Idara ya Mifugo na Uvuvi kwa kufanya doria za mara kwa mara katika maeneo mbalimbali ili kudhibiti vitendo hivyo. 


Alibainisha kuwa watuhumiwa 7 wanaoshikiliwa na Jeshi la Polisi watafikishwa mahakamani muda wowote kuanzia sasa ili sheria ichukue mkondo wake.


Aliongeza kuwa matumizi ya zana haramu za uvuvi ni hatari sana kwa rasilimali zilizoko katika mito na mabwawa kwa sababu hupelekea kukosekana kwa kitoweo cha samaki hivyo akatoa wito wa kukomeshwa kwa vitendo hivyo mara moja.  


Magiri aliitaka Idara ya Mifugo na Uvuvi kuendeleza doria hizo ili kuhakikisha zana haramu zote ikiwemo makokoro, nyavu, vyandarua na vinginevyo vinakamatwa na kuteketezwa ili kukomesha tabia hiyo.


Aidha aliwataka Wataalamu wa Idara hiyo kuendelea kutoa elimu kwa wananchi ili wajue vifaa vinavyoruhusiwa na visivyoruhusiwa kwenye uvuvi na athari za zana haramu kwa ustawi wa viumbe maji, huku akiwashauri kuhakikisha vifaa bora vya uvuvi vinapatikana kwa urahisi na kwa bei nzuri.


Awali Kaimu Mkuu wa Idara hiyo Mipawa Majebele alisema kuwa watuhumiwa hao walikamatwa kutokana na doria iliyofanyika katika maeneo mbalimbali kwa lengo la kudhibiti vitendo hivyo ambapo jumla ya nyavu haramu 276 na mashine 3 za kuvuta maji vyote vikiwa na thamani ya zaidi ya sh mil 100 vilikamatwa.


Alisisitiza kuwa doria hiyo ni muhimu sana kwa kuwa inasaidia kuokoa viumbe maji vilivyoko katika mito na mabwawa wilayani humo kwa kuwa ni rasilimali muhimu ambayo huchochea uchumi wa wananchi kupitia uuzaji samaki.


Alibainisha kuwa doria hiyo imesaidia sana kuongeza uzalishaji wa viumbe maji hivyo kutengeneza ajira kwa wavuvi 1219 ambao wameweza kujipatia kipato cha sh mil 100 na kuiwezesha halmashauri kuingiza kipato cha zaidi ya sh mil 33.


Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri hiyo Tito Luchagula alisema kuwa zoezi hilo litakuwa endelevu na wataweka utaratibu mzuri utakaosaidia wavuvi kufanya shughuli zao pasipo kubughudhiwa na mtu.


Alisisitiza kuwa hatua kali zitaendelea kuchukuliwa kwa wote watakaobainika kujihusisha na vitendo hivyo ambavyo huathiri kwa kiasi kikubwa mapato ya halmashauri ikiwemo kupunguza kitoweo cha samaki katika wilaya hiyo.

Monday, November 30, 2020

MAKALA :- AHADI ZILIVYOKUWA KWA WAGOMBEA KUHUSU HAKI ZA WATOTO

 




Na Robert Kakwesi

 

MCHAKATO wa kuwapata viongozi wa ngazi mbalimbali kwenye uchaguzi Mkuu mwaka huu unafikia mwisho tarehe 28 mwezi huu pale watakapopatikana viongozi watakaochaguliwa na wananchi.

 

Viongozi hao kuanzia madiwani,wabunge na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,watapatikana baada ya kufanyika kampeni iliyochukua miezi miwili kwa wagombea kunadi sera za vyama vyo kwa lengo la kuwashawishi wananchi wawachague.

 

Katika wagombea wanaonadi sera za vyama vyao,wanaeleza kuwa Ilani za Vyama vyao kimsingi zinaeleza mambo muhimu atakayofanyiwa mtoto kuanzia mama yake anapokuwa mjamzito hadi anapozaliwa na kukua.

 

Mgombea waChama Cha Mapinduzi (CCM) jimbo la Tabora Mjini,Emmanuel Mwakasaka,anasema Ilani ya Chama chake inaeleza mtoto kupewa stahiki zake kwa kuangaliwa mzazi wake ambaye anapatiwa huduma tangu awapo tumboni.

 

Anasema kuwa mzazi anapatiwa chanzo kwa mujibu wa sera ya Afya ambayo inahimiza kila mjamzito kupata chanjo mbalimbali za kumkinga mtoto na magonjwa.

 

Anabainisha kwamba akinamama wajawazito kwa mujibu wa mwongozo wa Afya katika sehemu za kutolea huduma kuwa hawatakiwi kutozwa chochote kwani huduma za kujifungua ni bure.

 

Hata hivyo, anasema kuna athari za kupata mtoto kimakuzi kama hataandaliwa msingi mzuri katika makuzi yake na hilo chama chake imeliona na ndio maana kuna sera na miongozo mbalimbali ya kushughulika na watoto.

 

“Hili la watoto chini miaka mitano kuhudumiwa bure na wazee ni maalum kuhakikisha watoto wanapata makuzi mazuri ili wawe raia wema baadaye wenye afya njema,” anasema.

 

Mgombea udiwani wa kata ya Kanyenye,Manispaa ya Tabora,Donatus Rupoli,anasema chama chake cha Chadema, kinatoa msisitizo kwa watoto kupata huduma bora katika makuzi yao kuanzia nyumbani hadi awapo shuleni.

 

Anasema hawataki mtoto akue katika mazingira mabaya kwa vile wanajua athari zake kuwa anaweza kudhurika kiafya na kushindwa kutoa mchango wake kwa Taifa ipasavyo.

 

Anasema akiwa diwani atahakikisha watoto wanapata huduma bora tangu wanapozaliwa na hata kabla ya kuzaliwa ili wakue katika makuzi mema na kuwa na afya nzuri.

 

Mkazi wa kata ya Ng’ambo,Zubery Abdallah,anasema bahati mbaya sana wagombea wengi katika nafasi za udiwani,ubunge na hata urais hawaelezi kuhusu namna watakavyoshughulika na mtoto kimakuzi.

 

“Tunataka watueleze ni kwa namna gani watatuhakikishia watoto wetu wanapata makuzi bora na sio tu kusema matibabu bure,” anasema

 

Naye Lucas Yohana mkazi wa Chemchem,anabainisha kwamba kwa sasa watoto wanapata chanjo kwa uhakika jambo wanalolifurahia, ingawa dawa kwa watoto wadogo chini ya umri wa miaka mitano ni tatizo.

 

Anaeleza kwamba serikali imeweka mwongozo mzuri wa watoto wa umri huo kupata matibabu bure, lakini kiuhalisia hilo halifanyiki katika sehemu za kutolea huduma za afya,” anasema.

 

“Ukienda vituo vya kutolea huduma unaambiwa hakuna dawa labda panadol tu sasa hili halijaa vizuri,” anasema.

 

Anasema kama matibabu ni bure basi na madawa yawe yanapatikana vinginevyo ni kiini macho, kwani kama mzazi hana fedha,afya ya mtoto inakuwa mashakani.

 

Kwa ufupi wazazi wanataka wahakikishiwe uhakika wa watoto kupata ulinzi kimatibabu kuanzia pale mimba inapotungwa hadi angalau anapofikisha umri wa miaka mitano

 

Daktari wa watoto katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tabora,Kitete,Dk. Mnubi Baguma,anasema kuna athari kubwa kwa watoto ambao hawalelewi katika mazingira mazuri na salama.

 

Anasema mtoto mbali ya kutakiwa kulelewa katika mazingira mazuri,anapaswa kupata maziwa ya kutosha kutoka kwa mama yake na kama mama atakuwa  na msongo wa mawazo,kamwe hawezi kutoa maziwa ya kutosha.

 

“Maziwa ya mama pia hutegemea saikolojia yake achilia mbali chakula anachokula,” anasema.

 

Anaeleza kuwa kuna athari kwa mtoto anayelelewa katika mazingira yasiyo salama kwa vile athari zake kimakuzi ni mbaya kwani anaweza kuwa mzito darasani kujifunza ukilinganisha na yule anayelelewa katika mazingira mazuri. “Maziwa ya mama kwa kipindi cha miezi sita yanatengenezwa kwa namna yake kiasi kwamba mahitaji yote ya mtoto yapo yakiwemo maji,” anasema.

 

Dk. Baguma anaeleza kwamba baada ya miezi sita ndiyo mtoto anaweza kuanza kupewa vyakula vingine huku akiendelea kunyonya hadi anafikisha miaka miwili au mitatu kutegemea hali yake.

 

Anaeleza kwamba mtoto huanza kujengwa tangu mimba inapoingia, ambayo ni msingi mkuu wa maisha yake,yanayoendelea pale mimba inapokua kisha kuzaliwa hadi anafikisha miaka mitatu hadi mitano.

 

“Msingi mkubwa wa mtoto kimakuzi na kiakili huanza kujengwa mimba inapotungwa,kulelewa hadi kuzaliwa na kuendelea wakati akinyonya mpaka anapoacha kunyonya,” anasema.

 

Ni dhahiri kuwa msingi wa makuzi ya akili ya mtoto anayeishi katika mazingira magumu unakuwa haupo vizuri,ambapo hupata msingi mbaya wa maisha yake.

 

Anasisistiza kuwa akili ya mtoto humuathiri hata akikua na kuanza shule kwani anakua hajiamini na kujitenga sababu anakuwa anajengwa na kuathirika akiwa tumboni au baada ya kuzaliwa,akiongeza kuwa mara nyingi huathirika hadi utu uzima wake.

 

Kutokana na athari za mtoto kitaalamu kwa mujibu wa Dk. Bagumani vizuri kwa wagombea siyo tu kuweka msingi mzuri kwa makuzi ya mtoto bali hata mazingira ya wazazi watarajiwa na wazazi wenye watoto.

 

Mtaalamu wa elimu ya malezi kwa makuzi ya mtoto,Ofisa Muuguzi katika zahanati ya Mjini Tabora,Catherine Mushi,anasema elimu hiyo ni muhimu kwa vile inamsaidia kukua kimwili,kiakili,kihisia na kijamii. Anaeleza kuwa elimu hiyo huanzia tangu ujauzito hadi umri wa miaka mitatu.

 

Mushi anabainisha kuwa mtoto anajifunza kutambua rangi na vitu mbalimbali,akisisitiza elimu ya utambuzi huanzia nyumbani na siyo sehemu nyingine yoyote,jambo linalodhihirisha watoto walio mahabusu au gerezani hukosa fursa hiyo muhimu.

 

Anabainisha kuwa pamoja na wazazi kutakiwa kuzungumza na watoto wao wangali tumboni na baada ya kuzaliwa,bado wanahitajika kucheza nao michezo mbalimbali na kuwaimbia.

 

Ni wazi kuwa kwa mama mwenye msongo wa mawazo anayeugua ugonjwa wa sonona,kutokana na madhila aliyopata,hawezi kufanya hayo kwa mtoto kutokana na hali yake na mazingira na hivyo kumkosesha msingi mzuri wa makuzi yake.

 

Mushi anabainisha kuwa tafiti za watoto zinaonesha wale waliopewa msingi bora wa malezi kuanzia utungwaji mimba,inapolelewa hadi anapotimiza miaka mitatu,huwa na tabia nzuri na hazibadiliki hata wakiwa wakubwa.

 

Mwanasheria wa asasi isiyo ya Kiserikali ya Jamii Salama Development Volunteer,JSDVambayo inajishughulisha na utoaji elimu ya sheria kwa wasaidizi wa kisheria,Paralegal,Charles Ayo,anasema sheria ya mtoto ya mwaka 2009 inakataza mtoto kutwezwa au kushushwa utu wake. Wagombea wanapaswa kuhakikisha wanalinda haki za mtoto.

 

Anasisitiza kwamba watoto ni Taifa la baadaye na kama wakiwekewa msingi mzuri,watakuwa na manufaa kwa Taifa na kutaka wagombea na vyama vyao kutoa umuhimu katika makuzi na malezi ya mtoto.

 

Mkataba wa kimataifa wa watoto (CRC) wa mwaka 1989,unataka watoto kuanzia ujauzito hadi wafikishapo miaka mitatu kupata lishe bora, ulinzi na mahitaji bora kwa ajili ya makuzi yao na kuimarisha ubongo.

 

 Ni dhahiri kwamba kwa watoto wanapaswa kupewa haki haki zao kikamlifu ikiwamo kupata  lishe bora katika maisha yao.

 

Hivyo kutokana umuhimu wa mtoto ambaye ni Taifa la baadaye,kupata stahiki na haki yake ya kuishi katika makuzi bora na kulelewa vema na wazazi au walezi wao, wagombea pamoja na vyama vyao vya Siasa,wanapaswa kutambua kuwa jambo hilo ni muhimu na linalopaswa kuwekwa msisitizo katika Ilani za Vyama vyao,sera na mipango yao kama wagombea.

 

MAKALA - NAMNA WATOTO WALIVYOKUMBUKWA WAKATI WA KAMPENI

 


Kampeni za ucharguzi mkuu mwaka huu zinaendelea kwa wagombea wa vyama mbalimbali kunadi sera zao kwa lengo la kupata nafasi za uongozi kuanzia udiwani,ubunge na Urais.

 

Katika kampeni hizo zinazotarajia kukamilika tarehe 27 mwezi huu na hatimaye wananchi kupiga kura siku inayofuata,wagombea wa vyama mbalimbali,wamekuwa wakinadi sera zao kupitia majukwaa na wananchi kuwasikiliza.

 

Hata hivyo wapo wagombea katika manispaa ya Tabora ambao wanafanya kampeni za nyumba kwa nyumba pasipo kutumia majukwaa kutokana na wao wanachokieleza kuwa kuwa ni ukosefu wa fedha.

 

Kwa wale wanaonadi sera zao kupitia majukwaa,wamekuwa wakieleza umuhimu wa michezo kwa wananchi na hasa watoto wakiwemo wanafunzi.

 

Mgombea ubunge kwa tiketi ya Chadema,jimbo la Tabora mjini,Hawa Mwaifunga,katika kampeni zake,anaeleza kuwa atatoa kipaumbele katika michezo mashuleni kwa lengo la kuibua vipaji.

 

Anaeleza kwamba chama chao katika Ilani yake,kinaeleza kuwa watashughulika na watoto shuleni kwa kuhakikisha sio tu wanapata chakula shuleni bali pia hawasomi kwenye msongamano huku wakipewa fursa ya kushiriki michezo.

 

"Tunafahamu kwamba mtoto shuleni akishiriki michezo hata ubongo wako unakuwa vizuri na hilo tutalitilia maanani"Anasema

 

Mwaifunga aliyecheza netiboli akiwa shuleni,anasema michezo hasa katika shule za msingi itapewa umuhimu na yeye kuwa mstari wa mbele kuhamasisha sanjali na kutoa misaada ya vifaa ili watoto shuleni wafurahie michezo na kupenda masomo yao.

 

Anabainisha kwamba msingi mzuri wa mtoto kimichezo ni shule za msingi na kwamba wanataka vipaji viibuliwe kuanzia ngazi hiyo ya shule za msingi na kuimarishwa sekondari.

 

Mgombea ubunge wa jimbo la Tabora Mjini kupitia CCM,Emmanuel Mwakasaka,anasema katika ilani ya CCM,michezo inasisitizwa na kupewa umuhimu mkubwa kwani ni mojawapo ya ajira.

 

Anasema katika Ilani ya Chama chake,michezo imewekewa umuhimu mkubwa kwa vile,wanataka kuibua vipaji vya watoto na kuviendeleza na kwamba ndio maana kuna michezo katika shule za msingi na sekondari ambayo wanafunzi wanashiriki.

 

Anasema pamoja na ilani yao kusisitiza kuhusu michezo,hata yeye pia ni mdau wa michezo na kwamba atakuwa mstari wa mbele kutoa vifaa vya michezo kwa watoto na wanafunzi mashuleni.

 

"Tutahakikisha watoto wanacheza kwa vile ni moja ya haki yao ya msingi katika maisha yao na tutakuwa tunawawekea msingi mzuri wa kujipatia ajira pindi wakikua kama wanavyo vipaji"Anasema

 

Naye mgombea wa jimbo hilo,kupitia CUF,Mirambo Camir,anasema chama chao kupitia Ilani kinaeleza umuhimu wa mkwa watoto na kwamba hata yeye ni mpenda michezo.

 

Anasema watoto wakiwemo wanafunzi,hawatapata shida kwa vile yeye pia ni kocha wa mpira wa miguu,akiwa amefundisha timu mbalimbali za ligi kuu na madaraja ya kwanza hadi la pili.

 

Mirambo ambaye anatumia muda mwingi kueleza sekta ya michezo majukwaani kutokana na kuwa kocha ,anasema hiyo ndio fani yake ambayo atatitumia kuibua vipaji vya watoto shuleni pamoja na kufanya majukumu yake ya ubunge.

 

Mwalimu katika shule ya Msingi ,Ipyana Daud,anasema ni muhimu watoto wakapewa kipaumbele katika kuhakikisha wanajua fursa ya kushiriki na kunufaika kupitia michezo.

 

"Ni muhimu wakafahamu namna wawakilishi wao watakavyoifanyia sekta ya michezo ambayo kwa kweli ni muhimu kwa watoto shuleni"Anasema

 

Mwanafunzi wa shule ya msingi,Samson Lucas anayesoma darasa la saba,anaeleza kwamba haelewi kama wanapaswa kufahamu namna watakavyofanyiwa na viongozi wanaochaguliwa kwa vile yeye hajihusishi na Siasa.

 

Anasema hata katika mikutano ya siasa yeye huenda kwa lengo la kuangalia wasanii kama wapo na kusikiliza wanachosema wagombea inagwa huwa hakitilii maanani.

 

"Mimi naenda kwenye mikutano kama kuna wasanii tu,sehemu ambazo hawapo huwa siendi"Anasema

 

Kwa mujibu wa Sheria ya mtoto ya mwaka 2009,watoto wana haki mbalimbali ikiwemo ya kucheza kwa kushiriki pia michezo mbalimbali na kukutana pamoja na kujifunza.

 

Sheria hiyo ni muhimu sana kwa watoto na inatoa mwongozo wa namna ya kuwatendea watoto ikiwemo kushikiriki michezo.

 

Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora,Msalika Makungu,anasema mkoa unatoa umuhimu kwa watoto kushiriki michezo na hiyo ni kutokana na mikakati na mipango ya Serikali kuona umuhimu wa michezo.

 

Anabainisha kwamba wanataka wavumbue vipaji kuanzia ngazi za chini kwa maana ya shule za msingi na ndio maana wanatoa mafunzo kwa walimu wanaowafundisha watoto wadogo mashuleni.

 

Anaeleza kwamba katika kuthamini michezo mashuleni,ndio maana kuna mashindano ya  Michezo ya shule za msingi ambapo kunakuwa na michezo mbalimbali kuanzia kwenye shule,kiwilaya,mkoa na hadi Taifa kila mwaka.

 

Afisa michezo wa Mkoa wa Tabora,Josephat Ngazime,anasema wameweka mkakati wa kuandaa kanzi data za wanamichezo katika shule za msingi lengo likiwa ni kuwatambua na kuwatumia pale wanapohitajika.

 

Anasema wanataka kufahamu ni nani ni mahiri katika mchezo gani ili iwe rahisi kuwapata na kuwatumia wanapohitajika lakini pia kuviendeleza vipaji vyao.

 

Wakazi wa Manispaa ya Tabora,wanawapongeza wagombea ambao wanaweka kipaumbele michezo kwa watoto kwa vile ndio Taifa la kesho.

 

Ibrahim Hussein mkazi wa Kanyenye,anasema kwa kuwathamini watoto,wagombea wanaweka katika mazingira chanya kwani wanapomaliza masomo yao,watakuwa katika nafasi nzuri ya kutuia vipaji vyao wanapokuwa.

 

Naye Maimuna Seleman mkazi wa Isevya,anashukuru baadhi ya wagombea kuona umuhimu wa kukuza sekta ya michezo kwa vile ni ajira nzuri na inayolipa vizuri.

 

"Sasa hivi ajira serikalini ni tatizo kubwa hivyo tunaona sehemu ya kuwafanya watoto wetu wafanikiwe kimaisha ni kupitia sekta ya michezo"Anasema

 

Kampeni za Uchaguzi Mkuu mwaka huu,zinatarajia kumalizika tarehe 27 na uchaguzi kufanyika tarehe 28 mwezi huu huku ajenda mbalimbali zikielezwa na vyama vya Siasa kwa lengo la kuwashawishi wapiga kura wawachague.

 

CHAMA CHA SOKA MANISPAA YA TABORA CHAPATA BOSI MPYA

 


Mwenyekiti wa chama cha Soka Manispaa ya Tabora Samwel Malle akiwashukuru wajumbe wa mkutano mkuu wa uchaguzi kwa kumchagua yeye na viongozi wengine.Picha na Allan Ntana.


Na Allan Ntana, Tabora


CHAMA cha soka wilayani Tabora, Mkoani hapa (TUFA) kimepata viongozi wapya watakaokiongoza kwa kipindi kingine cha miaka minne baada ya kumalizika kwa uchaguzi wa Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti, Katibu na wajumbe wa Kamati tendaji.

Akiongea na gazeti hili baada ya kukamilika kwa uchaguzi huo na matokeo kutangazwa, Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi Pankras Kaikai Bwena alimtangaza Mwandishi wa habari za michezo wa kituo cha redio VOT FM Samwel Malle kuwa mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti kwa kupata kura 28 dhidi ya kura 21 alizopata mpinzani wake Amani Seifu.

Aidha Andrew Zoma aliibuka kidedea katika nafasi ya Makamu Mwenyekiti baada ya mgombea pekee aliyekuwepo kujitoa kwenye kinyang’anyiro hicho kwa madai ya kubanwa na majukumu mengine.

Bwena alimtangaza Mwalimu Awadh Sabuni Said kuwa Katibu wa chama hicho baada ya kupata kura za ndio 40 na nafasi ya Katibu Msaidizi akatangazwa Paschal Herman aliyekuwa mgombea pekee kwa kupata kura zote 40.

Aidha alimtangaza Abdallah Mgemwa kuwa Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa chama cha soka mkoa wa Tabora (TAREF) kwa kupata kura 31 dhidi ya 18 alizopata mpinzani wake Geofrey Mabele.

Kwa upande wa soka la wanawake, msimamizi alimtangaza Frola Kadamanja kuwa Mwakilishi wa TAREFA baada ya kupata kura za ndio 48, huku Henry Richard Kitundu akichaguliwa kuwa mwakilishi wa vilabu kwa kupata kura  za ndio 48.

Bwena alibainisha kuwa kwa nafasi ya ujumbe wa Kamati tendaji ya chama hicho ilichukuliwa na Willson Msonzela aliyepata kura 45 na Martin Enock aliyepata kura 48.

 

MAKALA - MANUFAA WALIYOPATA WATOTO WAKATI WA LIKIZO YA CORONA

 
Robert Kakwesi,Tabora


Makala-Manufaa waliyopata watoto wakati wa likizo ya Corona

                                                            

Tanzania kama nchi nyingine duniani ilipata wagonjwa wa Homa kali ya mapafu maarufu kama corona,ugonjwa uliochukua maisha ya mamilioni ya watu katika nchi mbalimbali Tanzania ikiwemo.

 

Sanjali na kuua watu,ugonjwa huo pia uliwafanya maelfu watu dunia kuugua na kufanya watu kubadili mfumo wa maisha kwa lengo la kuukwepa ugonjwa huo ambao ulielezwa hautaki msongamano wa watu.

 

Kutokana na athari zake,Tanzania iliachukua uamuzi wa kuzifunga shule zake zote kuanzia za awali hadi Vyuo Vikuu na wanafunzi kutakiwa kwenda likizo mwezi wa tatu hadi mwezi wa sita mwaka huu.

 

Wakati wa likizo,Serikali ilitoa maagizo kadhaa kwa watoto ikiwemo kukaa majumbani na kuwataka wazazi na walezi kuwaangalia kwa karibu watoto wao ili wasipate maambukizi ya ugonjwa huo hatari.

 

Kuna msemo usemao kuwa katika jambo baya pia kuna uzuri wake na ndio maana pamoja na ugonjwa huo kuchukua maisha ya watu na kuhatarisha uchumi wa nchi nyingi duniani kulikuwa na mazuri yake kwa watoto.

 

Dkatari wa watoto katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tabora,Kitete,Dr Mnubi Baguma,anasema mtoto anapopa muda mwingi wa kuwa na mzazi wake anapata furaha na amani na hivyo kukua vizuri.

 

Anasema malezi mazuri anayopata kutoka kwa wazazi wake yanamjenga kiakili na kuwa na ubongo unaochemka tofauti na mtoto asiyepata malezi mazuri na kula vizuri kutoka kwa mzazi wake.

 

Anabainisha kuwa mtoto anapokuwa mbali na wazazi wake,kisaikolojia huathirika kwani anakuwa najenga imani kubwa kwa wazazi wake na anaposononeka,anapata wakati mgumu na akili yake kuathirika kwa namna moja au nyingine na hivyo kuweza kuathirika pia kimasomo.

 

“Mtoto anayeishi vizuri na wazazi wake na kupata malezi bora,hata ukuaji wake na akili yake unakuwa tofauti na wengine wasiopata anayopata”Anasema.

 

Askofu wa Anglican Dayosisi ya Tabora,Elias Chakupewa,anasema katika kipindi cha likizo ya ugonjwa huo,wazazi na walezi walipata muda zaidi wa kuwasoma tabia watoto wao tofauti na kabla ya ugonjwa huo.

 

Anasema ni muhimu wazazi na walezi kuwa karibu na watoto wao kwa lengo la kuwafundisha tabia njema na kuwasoma mienendo yao.

 

Mzazi Lucas Simon,anakiri likizo ya ugonjwa huo kumfanya kuwa karibu zaidi na watoto wake na hivyo kuwafahamu tabia zao zingine ambazo alikuwa hazifahamu.

 

“Tulikuwa na wakati mzuri baada ya kuondolewa wasiwasi kuhusu ugonjwa huo na kwangu tulikaa vizuri sana na kufurahi na watoto wangu wa darasa la tano na la tatu”anasema

 

Mwanafunzi Hadija Baraka wa shule ya msingi Kitete,Manispaa ya Tabora anayesoma darasa la sita,anasema wazazi wake walichukua jukumu la kuwafundisha nyumbani tofauti na zamani.

 

Anaeleza kwamba hakuwahi kufundishwa na wazazi wake kwani anaporudi nyumbani hakuwa akiwakuta na wanaporudi inakuwa wakati wa usiku wao wakiwa wamelala.

 

“Wazazi wangu ni watumishi wanaosafiri sana lakini wakati wa likizo ya corona tulikuwa tunashinda nao nyumbani”Anasema

 

Mwanasheria Charles Ayo,anasema mtoto ana haki ya kucheza na kufurahi na kipindi cha likizo ya corona,watoto wengi walipata muda zaidi wa kucheza na kufurahi.

 

Kwa mujibu wa sheria ya mtoto ya mwaka 2009,mtoto ana haki ya kucheza na hilo wazazi walilitekeleza vizuri ingawa hawakupata muda mzuri wa kushiriki kikamilifu na wenzao.

 

Anabainisha kuwa kwa mtoto kucheza na kufurahi anapata amani ya moyo na hata akili na ukuaji wake unakuwa ni mzuri tofauti na wale wasiocheza au kushiriki furaha utotoni.

 

Mtaalamu wa saikolojia ya watoto,aliyeomba hifadhi ya jina lake,anasema malezi huchangia kwa kiasi kikubwa akili na ukuaji wa mtoto.

 

Anaeleza kuwa malezi anayopata mtoto ni kuanzia chakula anachokula,namna anavyolelewa katika maisha yake kuwa yanachangia kuwa na akili nzuri na mwili mzuri.

 

“We angalia watoto wasiolelewa vizuri wengi wanakuwa na utapiamlo na akili inakuwa ni changamoto”Anasema.

 

Anasisistiza kuwa wakati wa likizo ya corona,wazazi na walezi wale waliokaa  vizuri na watoto wao,watakuwa walichangia kuongezeka akili na ukuaji wao kikamilifu,akisistiza mtoto anafurahi kuwa karibu na mzazi wake.

 

Aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Tabora,Aggrey Mwanri,aliagiza watoto kufundishwa kupitia njia ye redio zilizopo Manispaa ya Tabora na watoto kujifunza.

 

Anasema pamoja na changamoto zake lakini ilisaidia kwa baadhi ya watoto kujifunza kwa njia hiyo jambo lilikuwa geni kwao kwa mara ya kwanza.

 

Mwanafunzi Iddy Hassan wa shule ya msingi Kanyenye,anasema hakuwa na utaratibu wa kusikilia redio lakini wakati wa likizo ya corona ndio aliweka katika ratiba yake kuwa anasikiliza redio.

 

“Hadi leo hii mimi ni mpenzi wa kusikiliza redio baada ya kujenga utamaduni wa kusikiliza redio katika vipindi vilivyokuwa vinafundishwa na kupata fursa ya kusikiliza vipindi vingine pia”Anasema

 

Aliyekuwa afisa elimu wa Mkoa wa Tabora,Suzan Nusu,anasema ufundishwaji wa vipindi kupitia redio ulikuwa haujazoeleka kwa wanafunzi wengi na ilikuwa changamoto kubwa kwao ambayo walijaribu kuitumia kwa manufaa yao.

 

Anasema kama ungeendelea kwa kipindi kirefu ilikuwa lazima mambo yaendelee na ndio maana waliamua kuwa na njia mbadala kujiandaa kikamilifu hata kama ungechukua muda mrefu.

 

Afisa elimu Manispaa ya Tabora,Joel Mkuchika,anasema wakati wa likizo ya corona,walikuwa wakiwasiliana na watoto na wazazi kikamilifu kwa lengo la kuwasaidia katika masomo na kujikinga na ugonjwa huo.

 

Anasema mawasiliano yalikuwa ya karibu zaidi tofauti na zamani na wazazi na walezi wengi walikuwa wakitaka kufahamu namna watoto wao watakavyoendelea kujifunza wakiwa nyumbani.

 

Kikubwa kwake ni kuona namna wazazi na walezi walivyouona ukweli wa kazi kubwa na nzuri inayofanywa na walimu katika kuwalea watoto wao wawapo shuleni.

 

Anasema wengi waliona ugumu wa kuwa na watoto wao nyumbani muda mwingi na kutupa pongezi kuwa tunafanya kazi nzuri sana nay a manufaa kwao na Taifa kwa ujumla.

 

Anabainisha kuwa somo walilojifunza wazazi na walezi kuhusu ugumu wa kuwatunza watoto ni furaha kwao kwani wana uhakika sasa watapata ushirikiano mkubwa zaidi kutoka kwao tofauti na zamani.

 

 

Serikali ya mkoa iliweka mkakati maalum kuhakikisha watoto hawapati maambukizi wakiwa nyumbani na hivyo kuweka mikakati mbalimbali ikiwemo kukataza watoto kutembea ovyo pamoja na wazazi na walezi kutakiwa kufuata masharti yote ya kujikinga na ugonjwa huo.

 

Nyumba zote zililazimishwa kuwekwa ndoo ya maji ya kunawa milangoni ili itumiwe na wote wanaopita pamoja na wale wanaoishi ndani ya nyumba husika.

 

Afisa ustawi wa Jamii Manispaa ya Tabora,Rehema Maembe,anasema wazazi na walezi wengi walikuwa hawatimizi wajibu wao kikamilifu na likizo hiyo, imewakumbusha kutimiza kikamilifu wajibu  kwa watoto wao.

 

Kutokana na baadhi ya manufaa ambayo wazazi na watoto wameyapata wakati wa likizo ya ugonjwa wa corona,ni imani kubwa kuwa kutakuwa na mabadiliko ya mahusiano kati ya wazazi/walezi kwa upande mmoja na walimu na pia watoto na wazazi/walezi wao kwa upande mwingine na hivyo kila mmoja kutimiza wajibu wake kwa manufaa yake na jamii kwa ujumla.

 

Kwa watoto kupata uzoefu tofauti na kulelewa na wazazi na walezi wao kwa muda mrefu,wanakuwa wamefurahi na kwa kujifunza kwa njia tofauti,kuimarisha ubongo na kupata akili zaidi huku wakiwa na uhakika wa kukua katika namna inayowaweka vizuri kimwili kutokana na malezi waliyopata na wanayoendelea kuyapata kutoka kwa wakubwa zao kiumri.