Featured Post

HALMASHAURI KALIUA YATOA MIKOPO SHILINGI MILIONI 240

MATANGAZO

Saturday, December 26, 2020

WADAIWA SUGU WA MAPATO MANISPAA TABORA KUSAKWA

Meya wa Halmashauri ya Manispaa Tabora Ramadhani Kapela (aliyeketi katikati) akimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa manispaa hiyo Bosco Ndunguru katika kikao cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo kiichofanyika hivi karibuni katika manispaa hiyo. Picha na Allan Ntana.
 



Na Allan Ntana, Tabora


HALMASHAURI ya manispaa Tabora inatarajia kuendesha msako maalumu kwa wadaiwa sugu wa mapato yatokanayo na ushuru ili kila mmoja alipe madeni yake, na watakaoshindwa kulipa watachukuliwa hatua za kisheria.


Hayo yamebainishwa juzi na Mkuu wa wilaya ya Tabora Mjini ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya hiyo Komanya Erick Kitwala alipokuwa akiongea na gazeti hili ofisini kwake.


Alisema kuwa licha ya wadaiwa hao kutakiwa kulipa madeni yao kwa wakati au kupunguza hadi watakapomaliza baadhi yao wamekuwa wakikwepa na wengine kutotoa ushirikiano jambo linalopelekea halmashauri kukosa mapato.


Alisisitiza kuwa mapato ya halmashauri ndiyo yanayofanikisha utekelezaji miradi ya maendeleo ya wananchi, hivyo hawezi kukubali watu waendelee kulimbikiza madeni tu pasipo kulipa.


Kitwala alibainisha kuwa baadhi ya watendaji wamekuwa hawatekelezi wajibu wao ipasavyo kwa kutofuatilia na kuchukua hatua stahiki kwa wale wote wanaokwepa kulipa mapato ya serikali, huku akionya kuwa Mtendaji yeyote atakayebainika kuwa chanzo cha upotevu wa mapato hayo atawajibika.


‘Tutafanza oparesheni maalumu ya kukusanya madeni kwa wadaiwa sugu wote katika maeneo mbalimbali ya manispaa, naomba kila mdaiwa sugu ajisalimishe mapema na kulipa deni lake kabla ya kuchukuliwa hatua ’, alisema.


Kwa upande wake Meya wa Manispaa hiyo Ramadhan Kapela alisema kuwa mapato mengi yamekuwa yakipotea kutokana na baadhi ya Watendaji wasio waaminifu na kutowajibika ipasavyo, hivyo akawataka kubadilika mara moja.


Alibainisha kuwa madiwani wana dhamana kubwa ya kusimamia mapato ya halmashauri hivyo akawataka kufuatilia zoezi la ukusanyaji mapato kwa Watendaji wa vijiji na kata ili watekelekeze wajibu ipasavyo.


Alibainisha kuwa miradi mingi inayotekelezwa na serikali inashindwa kukamilika kwa wakati kutokana na ufinyu wa bajeti, hivyo akawataka kuongeza kasi ya ukusanyaji mapato ikiwemo kufuatilia madeni yote ili yalipwe.


Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Tabora mjini Emanuel Mwakasaka aliwataka madiwani hao kuwa kitu kimoja na kuhakikisha mapato ya serikali yanayokusanywa yanatumika ipasavyo.


Aidha alishauri wale wote watakaobainika kukwepa kulipa kodi hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yao ili kuwezesha miradi mingi zaidi kutekelezwa ikiwemo kuwezesha vikundi vyote vya vijana, walemavu na akinamama wajasiriamali.


KANISA LA KCC LAMPONGEZA RAIS MAGUFULI


 Kwaya ya Wanaume (CMF) ya kanisa la TAG Kitete Christian Center lililopo katika manispaa ya Tabora wakiimba katika ibada maalumu ya Krismas iliyofanyika katika kanisa hilo. Picha na Allan Ntana.



Na Allan Ntana, Tabora


KANISA la TAG-Kitete Christian Center lililopo katika manispaa ya Tabora limempongeza Rais Dkt.John Pombe Magufuli kwa kumtanguliza Mungu katika utawala wake na kuliwezesha taifa kuvuka salama katika kipindi kigumu cha ugonjwa wa COVID 19.


Pongezi hizo zimetolewa jana na Askofu Mstaafu ambaye pia ni Mchungaji Kiongozi wa kanisa hilo Rev. Paul Meivukie katika ibada ya sikukuu ya Krismas iliyofanyika jana kanisani hapo.


Alisema kuwa katika sikukuu hii ya kuzaliwa Yesu Kristo jamii inapaswa kumshukuru Mungu kwa mambo makubwa aliyoyafanya katika taifa letu na kwa jinsi alivyomwongoza Rais Magufuli katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa homa kali ya mapafu (covid-19).


Alisema kuwa mioyo ya Watanzania wote inabubujika shukrani kwa Mungu kwa jinsi Rais wetu alivyosimama katika imani na kutangaza maombi ya siku 3 ya nchi nzima kuomba dua na sala na Mungu akasikia kilio chetu na kuliponya taifa.


Kwa upande wake Mchungaji Msaidizi wa kanisa hilo Rev Shadrack Herman aliwataka Watanzania kuendelea kumtumaini Yesu Kristo na kumpa nafasi katika maisha yao ili awalee na kuwapitisha katika magumu yote wasiyoyaweza.


Baadhi ya waumini wa kanisa hilo Dkt. Zefania Zenga, Jovent William, Peter Seme na Andrew Sebastian walisema kuwa Rais Magufuli ni kiongozi na mtumishi wa Mungu, imani yake imelibeba taifa na kuokoa roho za wananchi.


Walibainisha kuwa kama sio ujasiri na imani aliyonayo kwa Mungu ugonjwa wa corona usingeisha haraka kiasi hicho na watu wengi wangepoteza maisha kama inavyotokea katika mataifa mengine.


Walibainisha kuwa Mungu ni mweza wa yote hivyo wakaitaka jamii kuendelea kumtumaini katika kila jambo ili aendelee kutenda makuu ikiwemo kudumishwa amani, upendo na mshikamano hapa nchini.


Aidha waliitaka jamii kuendelea kuchukua tahadhari ya ugonjwa wa corona kwa kunawa mikono mara kwa mara huku wakisisitiza kumtanguliza Mungu katika kila jambo.


Aidha waliwataka waumini wa madhehebu yote ya dini kuendelea kumwombea Rais Magufuli na wasaidizi wake ili waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo na  kuharakisha maendeleo ya wananchi.

Monday, December 21, 2020

MADIWANI KALIUA WATAKIWA KUIGA KASI YA UTENDAJI WA JPM


 Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Kaliua Mkoani Tabora Raphael Lufungija (wa tatu kutoka kulia) akiongoza madiwani wenzake wa halmashauri ya wilaya hiyo kula kiapo cha uadilifu katika kikao cha baraza hilo kilichofanyika juzi wilayani humo. Picha na Allan Kitwe.



Na Allan Kitwe, Kaliua


MADIWANI wa halmashauri ya wilaya ya Kaliua Mkoani Tabora wametakiwa kuiga kasi ya utendaji wa Rais Dkt John Pombe Magufuli kwa kutekeleza wajibu wao kwa weledi mkubwa ili kuharakisha maendeleo ya wananchi wa kata zao.


Rai hiyo imetolewa juzi na Katibu Tawala wa wilaya hiyo Michael Nyahinga katika kikao cha kwanza cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo kilichoketi kwa ajili ya kumchagua Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa halmashauri hiyo.


Alisema kuwa kasi na weledi wa Rais Magufuli ni kielelezo kizuri sana kwa kiongozi yeyote yule anayetaka mafanikio, hivyo akawataka madiwani hao kutekeleza wajibu wao kwa wananchi kwa vitendo na sio maneno tu. 


Alisisitiza kuwa wananchi wanataka maendeleo na kutatuliwa kero zao na sio kuendekeza malumbano yasiyo na tija katika vikao vya baraza ambavyo ndivyo vyenye mamlaka ya kupitisha mipango ya maendeleo ya wananchi.


‘Nawapongeza madiwani wote mlioshinda katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu, uchaguzi umeisha sasa kila mmoja akatekeleze wajibu wake kwa vitendo na kwa kuzingatia kanuni, taratibu na sheria’, alisema.


Katibu Msaidizi Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Magharibi, Gerald Mwaitebele aliwataka kuzingatia maadili ya utumishi na kujiepusha kumiliki mali za udharimu huku akionya kuwa yeyote atakayeenda kinyume na kiapo hicho atachukuliwa hatua za kisheria.


Naye Mwenyekiti mpya wa halmashauri hiyo Japhael Lufungija ambaye ni diwani wa kata ya Ilege (CCM) aliahidi kusimamia kwa nguvu mapato ikiwemo kuibua  vyanzo vipya ili kuwezesha halmashauri hiyo kutekeleza miradi yake ya maendeleo.


Alisisitiza kuwa watashirikiana na serikali kuu kwa ukaribu zaidi ili miradi yote inayotekeleza kwa fedha za ruzuku au wahisani zitumike ipasavyo huku akionya mtumishi yeyote atakayetumia vibaya fedha hizo atakumbana na mkono wa sheria.


Makamu Mwenyekiti wa halmashauri hiyo Abdallah Hemed (diwani wa kata ya Ufukutwa) alisema ili kupata maendeleo makubwa, madiwani wote wanapaswa kushikamana na kushiriki ipasavyo katika suala zima la ukusanyaji mapato.


Aidha alibainisha kuwa utekelezaji wa ahadi walizotoa kwa wananchi utategemeana sana na kasi ya ukusanyaji mapato, hivyo akatoa wito kwa madiwani na watendaji wote kufanya kazi kama timu moja.



SIKONGE WAKAMATA ZANA HARAMU ZA UVUVI ZENYE THAMANI YA ZAIDI YA MIL 100


 Mkuu wa wilaya ya Sikonge Mkoani Tabora Peresi Magiri (mwenye suti nyeusi) akiwa na viongozi wenzake jana wakati wa zoezi la kuteketeza zana haramu za uvuvi zilizokamatwa na Maofisa wa Idara ya Mifugo na Uvuvi wilayani humo hivi karibuni. Picha na Allan Ntana 


Na Allan Ntana, Tabora


HALMASHAURI ya wilaya ya Sikonge Mkoani Tabora imekamata zana haramu za uvuvi zenye thamani ya zaidi ya sh mil 100 na watu 7 waliokuwa wakijihusisha na vitendo hivyo wanashikiliwa na jeshi la polisi kwa tuhuma za kusababisha uharibifu mkubwa wa viumbe maji.


Akizungumza na vyombo vya habari jana Mkuu wa wilaya hiyo Peresi Magiri alipongeza halmashauri hiyo kupitia Idara ya Mifugo na Uvuvi kwa kufanya doria za mara kwa mara katika maeneo mbalimbali ili kudhibiti vitendo hivyo. 


Alibainisha kuwa watuhumiwa 7 wanaoshikiliwa na Jeshi la Polisi watafikishwa mahakamani muda wowote kuanzia sasa ili sheria ichukue mkondo wake.


Aliongeza kuwa matumizi ya zana haramu za uvuvi ni hatari sana kwa rasilimali zilizoko katika mito na mabwawa kwa sababu hupelekea kukosekana kwa kitoweo cha samaki hivyo akatoa wito wa kukomeshwa kwa vitendo hivyo mara moja.  


Magiri aliitaka Idara ya Mifugo na Uvuvi kuendeleza doria hizo ili kuhakikisha zana haramu zote ikiwemo makokoro, nyavu, vyandarua na vinginevyo vinakamatwa na kuteketezwa ili kukomesha tabia hiyo.


Aidha aliwataka Wataalamu wa Idara hiyo kuendelea kutoa elimu kwa wananchi ili wajue vifaa vinavyoruhusiwa na visivyoruhusiwa kwenye uvuvi na athari za zana haramu kwa ustawi wa viumbe maji, huku akiwashauri kuhakikisha vifaa bora vya uvuvi vinapatikana kwa urahisi na kwa bei nzuri.


Awali Kaimu Mkuu wa Idara hiyo Mipawa Majebele alisema kuwa watuhumiwa hao walikamatwa kutokana na doria iliyofanyika katika maeneo mbalimbali kwa lengo la kudhibiti vitendo hivyo ambapo jumla ya nyavu haramu 276 na mashine 3 za kuvuta maji vyote vikiwa na thamani ya zaidi ya sh mil 100 vilikamatwa.


Alisisitiza kuwa doria hiyo ni muhimu sana kwa kuwa inasaidia kuokoa viumbe maji vilivyoko katika mito na mabwawa wilayani humo kwa kuwa ni rasilimali muhimu ambayo huchochea uchumi wa wananchi kupitia uuzaji samaki.


Alibainisha kuwa doria hiyo imesaidia sana kuongeza uzalishaji wa viumbe maji hivyo kutengeneza ajira kwa wavuvi 1219 ambao wameweza kujipatia kipato cha sh mil 100 na kuiwezesha halmashauri kuingiza kipato cha zaidi ya sh mil 33.


Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri hiyo Tito Luchagula alisema kuwa zoezi hilo litakuwa endelevu na wataweka utaratibu mzuri utakaosaidia wavuvi kufanya shughuli zao pasipo kubughudhiwa na mtu.


Alisisitiza kuwa hatua kali zitaendelea kuchukuliwa kwa wote watakaobainika kujihusisha na vitendo hivyo ambavyo huathiri kwa kiasi kikubwa mapato ya halmashauri ikiwemo kupunguza kitoweo cha samaki katika wilaya hiyo.